Saturday, December 27, 2008

ZFA yatangaza kikosi cha Karume Boys

Chama cha Soka Zanzibar (ZFA), kimetangaza majina ya wachezaji wanaounda kikosi cha Karume Boys kinachokwenda kushiriki michuano ya Kombe la Chalenji kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati inayotarajia kuanza Jumatano ijayo Kampala, Uganda.

Kwa mujibu wa msemaji wa ZFA, Maulid Hamad Maulid alisema kikosi hicho kinatarajia kuondoka Jumatatu saa sita mchana kuelekea Uganda. Aliwataja wachezaji hao kuwa ni Mohamed Abdalla, Said Nassor, Haji Abdi, Nadir Haroub (nahodha msaidizi), Ismail Khamis, Haji Ramadhan, Ramadhan Khamisi, Suleiman Kassim na Mohamed Seif.

Maulid aliwataja wengine kuwa ni nahodha wa timu hiyo, Abdi Kassim, Ali Hamza, Juma Mohamed, Ali Mussa, Aggrey Morris, Abdullah Seif, Omar Ali, Abdulghan Gulam, Zubeir Juma na Amour Suleiman.

Alisema timu hiyo itaongozwa na Mkuu wa Msafara Ally Suleiman Shihata, Suleiman Amour ambaye ni Makamu wa Rais ZFA-Pemba, Masoud Atai (ZFA), Badr-El-Din (kocha mkuu), Ramadhan Bundala (kocha msaidizi), Ally Ferej Tamim (mjumbe wa Cecafa) na Makame Mpoma (mwamuzi msaidizi-Cecafa).

Maulid alisema kuwa kikosi cha Karume Boys kinatarajia kuagwa na kukabidhiwa bendera leo saa nne kwenye ofisi za ZFA. Karume Boys imepangwa kundi moja na ndugu zao, Tanzania bara, Somalia, Rwanda na wenyeji Uganda na inatarajia kuanza kampeni zake Januari 1, mwakani kwa kucheza na Somalia.

No comments:

Post a Comment