Thursday, December 11, 2008

Majambazi yavamia dar, yapora na kuua mmoja

Tukio la aina yake la ujambazi limelitikisa Jiji la Dar es Salaam leo asubuhi baada ya watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, kufyatuwa risasi kibao.

Inasemekana mtu mmoja amepoteza maisha katika tukio hilo na wengine kadhaa kujeruhiwa.

Walioshuhudia tukio hilo wanasema majambazi hayo matatu yalikuwa kwenye gari ndogo yakitokea eneo la Manzese huku mbele kukiwa na gari nyingine ambayo ilikuwa imebeba mabulungutu ya pesa kupeleka benki.

``Inavyoonekana, gari la majambazi lilianza kufutilia gari la pesa kuanzia mbali kabisa.

Yalipofika pale Magomeni karibu na kituo cha mafuta cha Gapco, lile gari la pesa likaingia kituoni hapo, lile la majambazi nalo likafuatia,``mmoja wa watu walioshuhudia tukio hilo alisema.

Kwa mujibu wa mashuhuda hao, punde tu baada ya magari hayo kuingia kituo cha mafuta, yale majambazi ghafla yalichomoa silaha na kurusha risasi hewani, kitendo kilichowafanya watu kutimka huku na huko kusalimisha maisha yao.

Imeelezwa kuwa majambazi hayo baada ya kuridhika hakuna watu karibu, yalimimina risasi nyingine kwenye kioo cha gari lenye pesa na kisha yakampiga risasi mlinzi aliyekuwa kwenye gari hilo.

``Risasi nyingine ziliendelea kurushwa ovyo ovyo na baadhi zikampata dereva wa gari hilo ambaye alijeruhiwa kwenye mkono,`` mmoja wa mashuhuda amedai.

Taarifa zaidi zimedai kuwa baada kutembeza risasi, majambazi hayo yalijitoma kwenye gari lenye pesa, kubeba minoti na kisha hayoo yakarudi kwenye gari yao na kuyoyoma kurudi njia ya Manzese.

``Yaliondoka taratibu bila hata haraka....utadhani yalikuwa yamewazindika polisi...si unajua pale kuna kituo cha polisi, lakini hakuna hata askari aliyeshtuka na kuja kwenye tukio,`` shuhuda mmoja amedai.
Hata hivyo haikuweza kufahamika ni kiasi gani cha pesa kimeibwa.

No comments:

Post a Comment