Sunday, February 15, 2009

Mwalimu Asimulia Bakora Alizopata Kutoka Kwa Mkuu Wa Wilaya

Mmoja wa walimu waliocharazwa viboko Jumatano iliyopita asubuhi mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Albert Mnali, ni mwalimu Ativus Leonard (33) wa shule ya msingi Katerero.

Akizungumza na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) juzi, Leonard alisimulia kuwa siku hiyo Mkuu wa Wilaya alifika shuleni kwao na kufanya mkutano na Mkuu wa Shule na walimu wengine.

Katika mkutano huo, Mkuu wa Wilaya aliwaambia kuwa amekuwa akifuatilia walimu wanaochelewa kufika kazini. "Alisoma majina ya walimu waliokuwa wakituhumiwa. Nilikuwa mmoja wao. Nilichelewa mara mbili kufika kazini mwezi uliopita," alikiri Mwalimu Leonard.

Baada ya kusoma majina hayo, kila mmoja aliulizwa atoe sababu za kuchelewa, ndipo yeye alipomwambia kuwa sababu zilitofautiana, yawezekana kuwa za kifamilia au ugonjwa. Ndipo Mkuu wa Wilaya akawambia tabia yao ya kuchelewa ilikuwa inaathiri maendeleo ya shule na kuifanya kushika mkia katika taaluma, jambo ambalo halikubaliki.

"Akasema atatuadhibu sawia. "Kwanza nilidhani anatania. Nikajiambia kuwa hilo halitawezekana...kwa kweli tangu hili litokee nimeshindwa kabisa kufundisha," alisema Mwalimu Leonard. Alisema lakini milango ya chumba cha walimu ilipofungwa na walimu kupangwa tayari kupokea adhabu ya viboko, ndipo mwalimu huyo alipoamini kuwa kumbe linawezekana.

"Walimu wenzetu saba wa kike, walichapwa viganjani, ilipofika zamu yangu, ofisa wa Polisi akaniamuru nilale chini ili nipate adhabu yangu. Nilikataa, lakini alinipiga mtama nikaanguka," alisema Leonard. Alisema wakati akiwa chini, polisi huyo aliendelea kumpiga kwa fimbo kubwa.

"Alinipiga kila mahali; miguuni, kifuani, mikononi. Alipomaliza, nilikwenda hospitalini kwa matibabu. Nilipewa dawa lakini bado nasikia maumivu kifuani," alilalamika. Alisema aliumia miguu pia, lakini kinachomuuma zaidi ni kuwa aliathirika kisaikolojia.

"Hii imenifanya nione aibu kukutana na wanafunzi. Hata kama hawakuniona nachapwa, lakini wanajua nini maana ya kuchapwa," alisema. Alisema ameshindwa kufundisha kwa sababu sasa anajisikia mnyonge mbele ya wanafunzi wake.

"Nimeoa na nina watoto wanne. Mke wangu naye ni mwalimu katika shule tofauti na yangu. Amekasirika kusikia kuwa nimefanyiwa hivi," alisimulia. Alisema mpaka sasa bado ana hasira na ameshikwa na bumbuwazi na haelewi kilichotokea. Pamoja na Mkuu wa Wilaya kuadhibiwa, lakini naye anatafuta jinsi ya kufidiwa na serikali kwa machungu yaliyompata.

Naye Phinias Bashaya, anaripoti kutoka Bukoba, kwamba siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kumvua madaraka Mnali, Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Mkoa wa Kagera, kimekiri kuwa baadhi ya walimu walisingizia kucharazwa viboko na mkuu huyo, ili kuwaunga mkono walimu wenzao.

Kauli hiyo imekuja baada ya viongozi wa chama hicho kuombwa kuthibitisha idadi halisi ya walimu waliocharazwa viboko baada ya vyombo vya habari kuripoti idadi tofauti ya walimu waliodaiwa kukumbwa na tukio hilo.

Wakizungumza katika ofisi zao mjini hapa jana, Katibu wa Mkoa, Aaron Masalu, alisema waliupokea kwa furaha uamuzi wa Rais na kuupongeza na kukiri kuwa walitembelea shule zilizohusika na tukio hilo na kuambiwa na walimu kuwa hata ambao hawakucharazwa nao waliingia katika mkumbo.

Alisema baada ya kugundua hali hiyo ya kutofahamu idadi halisi ya walimu waliocharazwa huku walimu wote wakidai kuchapwa, ilibidi viongozi hao na walimu wakubaliane waandaliwe walimu wenye uwezo wa kujieleza na kufafanua mazingira ya tukio lenyewe hata kama hawakuhusika na adhabu hiyo.

Akitetea hali hiyo, Mwenyekiti wa CWT, Dauda Bilikesi, alitolea mfano wa mtoto anayeweza kukunja ngumi kumtishia mzazi wake, hali ambayo alisema lazima itafsiriwe kuwa mtoto huyo alimpiga mzazi wake hata kama hakumgusa.

Naye Mwenyekiti wa CWT Wilaya ya Bukoba Vijijini, Gosbert Mashasi, mbali na kuungana na viongozi wenzake, pia alikiri upungufu miongoni mwa walimu na kusema wanaipongeza hatua iliyochukuliwa na Rais dhidi ya Mkuu wa Wilaya. Wakitoa maoni yao kuhusu hatua ya kuvuliwa madaraka kwa Mkuu wa Wilaya baadhi ya wakazi wa Kagera wakiwamo viongozi, walikuwa na maoni tofauti.

Florian Kaiza (34) mfanyabiashara wa mjini hapa aliupongeza uamuzi wa Rais akisema unafaa kwani kilichofanyika ni udhalilishaji mkubwa dhidi ya walimu. Aliongeza kuwa walimu walishapata jibu walilolihitaji na kuwaasa kuwa hakuna haja ya kuandamana badala yake watulie na wafanye kazi bila kuvunjika moyo, akiungwa mkono na Diwani wa Kasharunga, Muleba, Ponsian Rweyemamu (43), aliyeongeza kuwa yapo masuala mengi nchini yanayohitaji uamuzi wa haraka kama alivyofanya Rais.

Akizungumza kwa simu, Mwalimu Leonard ambaye pia ni Katibu wa Chama cha walimu kwenye shule hiyo, alisema alifarijika na uamuzi dhidi ya Mkuu wa Wilaya na kusema sasa walimu watulie na kufanya kazi. Tofauti na wengine kijana aliyejitambulisha kwa jina la Kraish Ally (32) wa mjini hapa, alisema Mkuu wa Wilaya ameonewa, akidai kuwa walimu wamewachosha wazazi kwa utoro na kutofundisha.

Alisema walimu wamekuwa wa kwanza kuvunja haki za watoto ambao wanastahili kufundishwa na badala yake kutanguliza miradi yao aliyosema inaendeshwa hata shuleni wakati wa masomo. Juzi Rais Kikwete alichukua hatua ya kumvua madaraka Mkuu huyo wa Wilaya kwa kuvunja Kanuni ya Sheria za Utumishi wa Umma na kuidhalilisha Ofisi na Mamlaka ya Ukuu wa Wilaya.



No comments:

Post a Comment